Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh Hemed Suleiman Abdulla ameuagiza Uongozi wa Hospital ya Abdalla Mzee Mkoani Pemba kuhakikisha ndani ya kipindi cha mwezi mmoja wamenunua mtambo mpya wa kuchomea takataka za Hospital ili kuepusha kusambaa kwa takataka jambo ambalo linaweza kusababisha kujitokeza kwa mardhi ya milipuko Hospitalini hapo.
Akikagua uendeshaji na utoaji wa huduma katika Hospitali ya Abdulla Mzee Makamu wa Pili wa Rais amesema Uongozi wa Hospital hiyo unatakiwa kujipanga katika kuhakikisha huduma zote muhimu zinapatikana Hospitalini kwa wakati unaostahiki.
Aidha Mhe.Hemed amesema amefarijika sana kuona huduma ya usafishaji wa figo(DIALYSIS) ULTRASOUND, EXRAY na huduma nyingine za maabara zinapatikana bila ya malipo pamoja na kuwepo kwa dawa za kutosha kwa wagojwa wanaopatiwa matibabu jambo ambalo ndio dhamira ya Rais Dkt. Hussein Mwinyi.
Kwa upande mwingine Makamu wa Pili wa Rais amemuagiza Afisa mdhamini Wizara ya Afya kushughulikia kwa haraka maslahi na stahiki za wafanyakazi ili kuwapa moyo wa ufanyaji wa kazi kwa kuwapatia wagonjwa huduma bora bila ya usumbufu wowote.
Wakati huo huo Makamo ya wa Pili wa Rais alikagua mradi wa Skuli ya Msingi Chanjaani Jombwe na Skuli ya Sekondari Ole (G+3 ) zinazojengwa na Mkandarasi Kampuni ya Mwinyi Building Contraction na Bench mark & Engineering Ltd ambazo zipo katika hatua za mwisho kukabidhiwa kwa Serikali.
Amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuekeza katika Sekta ya elimu kwa kuhakikisha inaweka miundombinu bora ya elimu ili wanafunzi wasome katika mazingira mazuri yatakayotoa wataalamu wabobezi wa fani mbali mbali ambao watakuja lisaidia Taifa kwa kufanya kazi ndani na nje ya nchi.
Sambamba na hayo Mhe. Hemed amewataka wazazi na walezi kulipa kipaombele suala la kuwapatia elimu bora watoto wao pamoja na kuwalea katika maadili mema yatakayowalinda na kujiingiza katika vitendo viovu.
Nae Naibu Waziri waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe. ALI ABDULGHULAM HUSSEIN amesema malengo ya Serikali kupitia Wizara ya elimu ni kuhakikisha inakamilisha miradi yote inayojengwa, kuongeza idadi ya madarasa na kujenga dahalia za kisasa ili ifikapo Januari 2025 wanafunzi wote wanaingia mkondo mmoja wa masomo.
GHULAM amefahamisha kuwa vifaa vyote vya kujifunzia na kufundishia ikiwemo viti, meza, kompyuta, na vifaa vya maabara vipo tayari na vitakabidhiwa mara tu baada ya kukamilika kwa ujenazi huo ndani ya mwezi wa Nane.
Kwa upande wao wakandarasi wanaojenga miradi hio Mwinyi Building Contraction na Benchimark Engineering Ltd wamesema wapo katika hatua za mwisho kukamilisha ujenzi huo ambapo wanatarajia kukuabidhi Serikalini mwishoni mwa mwezi wa nane ili wanafunzi waendelee na masomo yao katika mazingira mazuri na salama.
Wamesema wamechukua jitihada kubwa katika kuhakikisha wanajenga skuli hizo kwa viwango vilivyokubaliwa ili skuli hio ziweze kudumu na kutumika muda mrefu pasipo serikali kupata hasara ya kufanya ukarabati wowote.
Miradi iliyotembelewa na kukaguliwa na Makamu wa Pili wa Rais ni HOSPITAL YA ABDALLA MZEE MKOANI, KUKAGUA UJENZI WA SKULI YA GHOROFA MWAMBE, UJENZI WA BARABARA YA UKUTINI MTANGANI, UJENZI WA SOKO LA SAMAKI NA MBOGA MBOGA VITONGOJI, UJENZI WA KITUO CHA KUCHOMEA TAKATAKA VITONGOJI na KUKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA SKULI YA SEKONDARI YA GOROFA OLE.